Translate

Monday, August 6, 2012

MSICHANA AKATAA KUMTOA MAMA YAKE KAFARA


Msichana aliyeamua kuokoka, ameushangaza umati wa washirika wa kanisa moja la Kipentekoste lililoko Mtoni kwa Azizi Ally Jijini Dar es Salaam baada ya kueleza kuwa aliamua kuokoka na kujisalimisha kanisani hapo baada ya kakataa shinikizo la kumtoa kafara mama yake mzazi, huku tayari akiwa amewatoa kafara wadogo zake watano.

Kwa hekima gazeti Msemakweli limehifadhi jina la msichana huyo mwenye umri wa miaka 25 na Kanisa analosali hivi sasa ili kuepuka athari zinazoweza kumpata, kutokana na kudai kuhusika na vifo vya ndugu zake hao aliowaua kwa njia za kishirikina ambazo ni vigumu kuzithibitisha kwa njia za kisayansi, isipokuwa ukweli unabakia kwamba katika familia yake tayari wadogo zake watano wamekufa kiajabu ajabu katika vipindi tofauti!

Msichana huyo ambaye pia alifanya mahojiano maalum na Msemakweli hili hivi karibuni, alisema kilichomlazimisha ajisalimishe kanisani na kuokoka ni kitendo cha wachawi alioshirikiana nao kula nyama za wadogo zake watano aliyowaua na kuwatoa kafara, kumtaka amtoe kafara mama yake mzazi lakini akakata, ambapo walimweleza bayana kuwa watamtoa yeye kafara.
“Baada ya kuingizwa na bibi mzaa baba katika uchawi nikiwa na miaka tisa, nilitakiwa nikabidhiwe kiti na kuwa kiongozi wa wachawi na ndipo nikaanza kuwaua wadogo zangu na kuwala nyama nikishirikia na wachawi wenzangu”, alieleza msichana huyo.

Alisema alikuwa akiwaua wadogo zake hao kwa kuwanywesha dawa na kuwatupia mapepo ya magonjwa mbalimbali.
Msichana huyo alisema baada ya kuwaua kwa nyakati tofauti, aliwakabidhi kwa wachawi waliowachuna ngozi na kuwapika au kuwabanika, kisha kuliwa nyama.
Alisema wachawi wenzake nao walikuwa wakiua ndugu zao kwa zamu na nyama zao kutafunwa, kila kafara ya nyama ilipokuwa ikihitajika.
“Nakumbuka niliwaua wadogo zangu wakati nikiishi na wazazi wangu katika eneo la Kumpondenyali nchini Msumbiji ”, alisema msichana huyo ambaye kwa sasa anaishi Wilayani Mkuranga anakolelewa pia kiroho na kanisa alilookokea.

Alisema baada na kuchoshwa na tabia ya kuwaua wadogo zake na kula nyama zao, alikataa pia kumuua mama yake mzazi, ambapo wachawi wenzake walipotaka wamtoe yeye kafara, alimwendea mchungaji wa kanisa moja la Kipentekoste Wilayani Mkuranga na kumweleza kuwa ameamua kuachana na uchawi.

Baada ya Mchungaji kunikubalia, nilimwambia ningeleta zana zangu za uchawi ili zichomwe moto kanisani hapo’; jambo ambalo lilifanyika baadaye mbele ya waumini wa kanisa lake.

“Pamoja na binti huyo kutoa ushuhuda mrefu jinsi alivyokuwa akifanya uchawi, kuloga, kula nyama za watu na wachawi wenzake na wakati mwingine kujigeuza nyoka wakati akifanya kazi za ndani kwa mchungaji mmoja, aliwataka wachawi kuacha kuwatesa watu na kumrudia Mungu kwa usalama wa maisha yao kama alivyofanya yeye.
Alisema kimsingi anajutia sana mambo mabaya aliyokuwa akiyafanya ikiwa ni pamoja na kuwaua wadogo zake bila wazazi wake kujua chanzo cha vifo hivyo wakidhani ni magonjwa ya kawaida.
“Kwa kweli sikuona faida ya mambo hayo machafu…najisikia vibaya sana na kujuta na ndio maana nawasihi wachawi waache kuwatesa watu na waokoke. Nataka sasa niwe mtumshi wa Mungu nihubiri Injili kwa watu”, alisema msichana huyo.

Alisema wakati zana zake za uchawi zikichomwa moto kanisani, mama yake mdogo ambaye ni mchawi aliyekuwa akishirikia naye, alifika kanisani hapo na kufanya fujo akilalamika kwamba anaidhalilisha familia yao.
“Nakumbuka mchungaji alimkataza asifanye fujo na akaondoka huku akisema tutaonana nyumbani.Lakini hata hivyo bado Mungu ananilinda hadi leo.Kamwe sitarudi nyuma”, alisema msichana huyo.

Alibainisha kuwa Wakristo waliookoka na wasio legelege ni vigumu sana kuchezewa, kulogwa, au kuuawa na wachawi.
“Wakati nikifanya uchawi na wenzangu, Walokole walikuwa hawawezekani kabisa na kila tulipofika katika viwanja vya nyumba zao, tulikuta moto au wanajeshi wengi wakizilinda, hivyo hatukuwa tukiwaweza kabisa”, alisema msichana huyo.

No comments: