Translate

Friday, January 25, 2013

GARI LATEKETEZWA KWA MOTO HUKO KIJIJINI MSIMBATI BAADA YA KUTAKA KUMTEKA BIBI MWENYE MJI !!



MKUU wa Kaya ya Msimbati ambako gesi asilia inachimbwa mkoani Mtwara, Bibi Somoe Mtiti (106) amenusurika ‘kutekwa’ na mtu anayeaminika na wakazi wa eneo hilo kuwa ni mfanyakazi wa Idara ya Usalama wa Taifa baada ya wananchi kuvamia gari lake na kuliteketeza kwa moto jana usiku.

Hivi karibuni Bibi Mtiti aliionya Serikali juu ya mpango wake wa kusafirisha gesi ghafi kwenda Dar es Salaam kwa madai iwapo itapuuza onyo hilo bomba hilo litasafirisha maji badala ya gesi iliyokusudiwa.


Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Mtwara, Maria Nzuki alisema hana taarifa zozote kuhusiana na tukio hilo kwa kuwa mhusika hajakwenda polisi kulalamika.


Kwa mujibu wa wanakijiji hao, mtu huyo ambaye ana asili ya kijiji hicho waliyemtambua (jina linahifadhiwa) aliwasili kijijini hapo jana saa 10 jioni akiwa na gari dogo aina ya Mark II na kwenda nyumbani kwa shangazi yake.


Habari zinadai kuwa saa 2 usiku mshukiwa huyo alidaiwa kwenda nyumbani kwa Bibi Mtiti akiwa na gari pamoja na shangazi yake.
“Unajua yule bibi tunamlinda, sasa ilipoonekana ile gari usiku pale, watu wakaanza kujiuliza linafanya nini…wakaanza kusogea, kadiri muda ulivyokuwa unakwenda ndivyo watu walivyozidi kuongezeka,”alisema Juma Ayoub mkazi wa kijiji hicho.


Asha Hamisi ni mtoto wa pili wa Bibi Mtiti, akihadithia juu ya tukio hilo, alisema yapata saa 2 usiku wakiwa wanakula chakula walipokea wageni wawili ambao baada ya kumaliza kula waliomba kuongea na mkuu huyo wa kaya.


“Alikuja kijana na mama wakaniomba kuongea na bibi…alimuuliza bibi kama ana uwezo wa kwenda Mtwara, bibi akajibu hawezi…wakaniuliza mimi kama naweza kwenda badala yake nikawaambia siwezi…akasema ametumwa na Rais Jakaya Kikwete na Hawa Ghasia...wamjie bibi wakazungumze naye mambo ya gesi,” alisema Hamis.


Aliongeza kuwa “Kama bibi yupo tayari Jumanne ijayo watamfuata kwa gari…mimi nikasema sitaki…nilipochungulia nje nikaona watu wengi wamezunguka.”


Kwa upande wa mtoto mwingine wa bibi huyo alisema,” Kwa kuwa tunamfahamu tulimwambia aondoke mpango aliojia haufai, akawa anabisha, tukaendelea kumsihi..wakati huo watu wanazidi kuongezeka…alipotoka akakosea njia, alipopita hakukuwa na njia…watu walimfuata wakaanza kumrushia mawe…aliacha gari akakimbia…ndipo wananchi walipoliteketeza gari kwa moto,” alisema Manzi Mohamedi Faki mtoto wa tano wa Bibi Mtiti.


Shangazi wa mtuhumiwa amethibitisha kumpokea mwanaye huyo na kumsindikiza kwa Bibi Mtiti na ambako alimwomba mkuu huyo wa kaya akubali kuondoka naye kwenda Dar es Salaam kwa maelezo kuwa ametumwa na viongozi wake wa juu.

“Ni mwanangu mtoto wa kaka yangu, alikuja akaniomba nimepeleke kwa bibi akamsalimie tuliondoka saa 2 usiku…watu walituzingira na hali ilipokuwa mbaya niliondoka na kumwacha mwanangu pale, naye

alikimbia na ndipo walipochoma moto gari,” alisema shangazi huyo.
Alifafanua kuwa “Huyu mwanangu anaishi Dar es Salaam, anafanya kazi Usalama wa Taifa…nadhani alirudi jana hiyohiyo Mtwara.''

No comments: