Translate

Monday, March 25, 2013

JAMBAZI SUGU LAUWAWA KWA KUPIGWA RISASI




MTU mmoja ambaye anasadikiwa kuwa ni jambazi ameuawa kwa kupigwa risasi na Askari wa Jeshi la Polisi akiwa kwenye harakati za kuteka magari katika Eneo la Mlima Nyoka Jijini Mbeya baada ya kutokea kwa majibizano ya kurushiana risasi.
  
Jambazi huyo ni miongoni mwa watu waliokuwa wakitafutwa na Jeshi la Polisi Mkoani hapa akituhumiwa kuhusika na mauaji ya Askari Polisi mwenye namba G 68 PC Jafari yaliyotokea  Februari 6, Mwaka huu  katika eneo la Matundasi Wilayani Chunya.
  
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mbeya Diwani Athumani amethibitisha kutokea kwa tukio hilo katika Mkutano alioufanya na waandishi wa Habari Ofisini kwake ambapo alisema tukio hilo lilitokea  jana majira ya Saa 10(kumi) Alfajiri usiku wa kuamkia Machi 27, Mwaka huu.
  
Kamanda Diwani alisema kabla ya tukio majambazi wapatao wanne  tayari walikuwa wameweka mawe barabarani kwa nia ya kuteka magari ili wafanye uporaji katika eneo hilo la Mlima Nyoka ambalo limekuwa na matukio kadhaa ya watu kuporwa mali zao.
  
Alisema Jeshi la polisi baada ya kupata habari za kutegwa mawe, askari walifika kwa wakati kwa kuwa polisi walikuwa jirani na eneo hilo na kuweka mtego kwa kuwa majambazi hawakuwa wameonekana kwa wakati ule.
  
Aliongeza kuwa baada ya muda majambazi walipoona taa za gari walijitokeza tayari kushambulia lakini kabla ya hapo polisi walitoa amri ya kujisalimisha kinyume chake wakaanza kupiga risasi ovyo ndipo mashambulizi ya polisi yakafanywa.
  
Diwani alisema katika mapambano hayo alijeruhiwa jambazi mmoja kwa risasi kiunoni na ubavuni kulia na wengine watatu walifanikiwa kutoroka ambapo Marehemu alipowahishwa hospitali kwa matibabu daktari alibaini kuwa amekwisha fariki.
  
Alisema  jambazi huyo alikutwa na silaha moja SMG yenye namba  AB huku namba  nyingine zikiwa zimefutwa na magazine yake ikiwa na risasi ishirini na mbili (22) pamoja na mapanga mawili([2).
  
Aliongeza kuwa baada ya  Marehemu kufanyiwa upekuzi maungoni mwake jambazi huyo alikutwa na kitambulisho cha mkazi chenye namba B.0010453 chenye jina la Emanuel Blasius Mdendemi aliyezaliwa mwaka 1984 eneo la Matamba wilayani Makete Mkoa wa Iringa makazi yake ni Uwemba Mkoani Njombe.
  
“Jambazi huyu amebainika kuwa ni miongoni mwa majambazi waliokuwa kwenye mtandao wa majambazi uliokamatwa hivi karibuni kuhusiana na matukio waliyofanya Mikoa mbalimbali ikiwemo Mbeya,Njombe na Iringa.aidha amebainika kushiriki katika tukio la mauaji ya askari polisi PC Jafari wa kituo cha Mkwajuni – Chunya tarehe 06.02.2013.” Alisema Kamanda Diwani.
  
Aliongeza kuwa  ufuatiliaji wa majambazi waliotoroka unaendelea kufanywa ambapo pia  anatoa wito kwa yeyote mwenye taarifa za wahalifu hao azitoe bila kuchelewa kwa jeshi la polisi ili zifanyiwe kazi.

Pia  amewatahadhalisha majambazi na wahalifu wa makosa yeyote kuachana na uhalifu kwa kuwa ni biashara isiyo na faida badala yake wafanye shughuli halali kupata maendeleo ambazo fursa zake ni nyingi.

Picha na Mbeya yetu

No comments: